kwa nini maisha magumu?

         NINI KINASABABISHA UGUMU WA MAISHA? 

Maisha tunayoishi tunapaswa tuyafurahie na  tuishi  tukiwa na Amani, lakini kwa sababu moja au nyingine maisha huonekana kwamba ni magumu, maisha hayapaswi kuwa magumu kama tutaelewa ni vitu gani vinavyosabisha hali ya maisha ionekanae kuwa ngumu

Hapo chini nitaelezea kwanini maisha ya baadhi ya watu huonekana kuwa ya taabu na magumu hadi inafika kipindi mtu anakata tamaa ya kuishi

MAJUKUMU

Majukumu yanapaswa yaendane na uwezo wa kiuchumi katika maisha ya mtu, mtu anapokuwa ana majukumu mengi kupita uwezo wake wa kiuchumi hii hufanya mtu kuwa na hofu namna atakavyoweza kuituza familia au watu waliochini yake kwa mfano unakuta mtu ana watoto wawili halafu kazi hana au kipato chake ni kidogo mno

 Kuna aina mbili za majukumu

a)Majukumu ya lazima

haya ni majukumu ambayo kila mtu huwa nayo wewe kama kijana wa familia Fulani una jukumu la kusaidia ndugu zako au wadogo zako hapo nyumbani, majukumu kama haya kila mtu anayo na huwa hayaepukiki

 b)Majukumu ya kujitakia

Haya ni majukumu ya mtu binafsi kwa mfano ameamua kuoa na kuzaa watoto, ameamua kwenda sehemu za starehe na kutumia hela zake, amepigana na mtu sasa anatakiwa amlipe fidia au amekopa madeni kwa shida zake inabidi alipe, mara nyingi haya ndio majukumu yanayofanya maisha kuwa makumu kwa sababu wakati mwingine majukumu ya kujitakia huwa ni makubwa kuliko uwezo wa mtu 

       KUKOSA MAARIFA

Ukosefu wa maarifa ni changamoto kubwa sana, maandiko yanasema si vizuri nafsi ya mtu ikose maarifa, mtu aliyekosa maarifa ya namna ya kuyaboresha maisha yake hatoweza kuyabadilisha, hivyo ni lazima kujifunza namna ya kutatua changamoto za kimaisha na kujua ni namna gani utaweza kuongeza kipato chako, ili uweze kuyahimili majukumu uliyonayo

 KIPATO KIDOGO

Udogo wa kipato ni changamoto kubwa ambayo huwakatisha tamaa watu wengi, karibia kila mtu atakwambia hajaridhika na kipato anachopata au kwamba kipato chake hakikidhi mahitaji ya kifamilia , hivyo hupelekea mtu kupata shida na kutafakari atajikwamuaje katika maisha yake, ni vyema mtu kutafuta namna ya kuongeza kipato kwa kufanya biashara ndogondogo za pembeni 

Mara nyingi watu wengi ambao wameajiriwa hujiona kwamba wao tayari hawana tena haja ya kuwa na biashara nyingine lakini hii ni mbaya hakuna mtu aliyefanikiwa kwa kutegemea pesa za kuajiriwa ,tafuta mtaji uangalie ni kitu gani unaweza ukafanya kwa ajili ya kuongeza kipato chako 

KUSHINDWA KUWEKEZA PESA ZAKO

Kuwekeza pesa ni jambo la muhimu sana huwezi kufanikiwa kiuchumi kama huwekezi pesa zako, ndio kipato ni kidogo lakini je katika pesa unayopata huwa una wekeza kiasi gani kwa ajili ya malengo yako ya baadaye? Utagundua kwamba watu wengi huwa wahawekezi pesa na hawana pesa yoyote ya ziada kama likitokea tatizo la ghafla huwa wanaanza kuhaha ni wapi watapata fedha na mwisho wa siku wengi huishia kukopa madeni hivyo hupelekea hali ya maisha kuonekana ngumu.

 MTAZAMO HASI

Wapo baadhi ya watu wao kazi yao ni kufikiria vibaya kwenye kila jambo linalotokea, huwezi kufanikiwa kama mtazamo wako ni mbaya lazima ujifunze kuvitazama vitu katika mtazamo chanya kwa mfano limetokea tatizo jiulize tatizo hilo limesababishwa na nini na ni jinsi gani utalitatua na sio kususa, kutukana au kukata tamaa, unaweze ukakemea ukiwa na maneno chanya au kusema dukuduku lako pia kwa maneno chanya.

MAHUSIANO MABAYA NA WATU

Mahusiano yako na watu huchangia pakubwa katika maendeleo yako ukiona mtu amefanikwa ujue mahusiano yake na watu ni mazuri, hupaswi kutukana watu, au kuwakasirikia watu kwa mambo ya kawaida ongea na watu vizuri kama kuna changamoto tafuteni namna ya kuitatua ili mambo yaishe na mara nyingi vitu ambavyo huja katika maisha ya mtu huletwa kupitia watu waliomzunguka hivyo kama wewe mahusiano yako na watu ni mabaya basi utachelewa sana kufanikiwa maana kitu ambacho ungeweza kukipata kwa mtu Fulani kwa urahisi huwezi kukipata tena kwa sababu ya uhusiano mbovu baina yenu hivyo inabidi usubiri mpaka atakopopatika mtu mwingine mwenye hicho kitu

LAWAMA

Usitafute mtu wa kumlaumu katika maisha yako, ndio maisha yana changamoto labda haukuweza kusoma kwa sababu wazazi hawakuwa na pesa au walikuwa hawajali cha muhimu ni kutafuta kujua unatokaje kwenye hali ya maisha uliyo nayo, unapofanya kazi na watu acha kulalamika na kulaumu watu ovyo, lazima ujifunze kuwaonyesha watu kwamba wewe ni msaada kwao na kama itatokea kazi yoyote wanaweza wakakupata bila shida yoyote

Watu wengi wenye lawama hakuna anaeweza kufanya nao kazi kwa mtu mrefu kwa sababu linapotokea tatizo lolote wao huanza kujitoa na kutupia lawama watu wengine

 KUKOSA MAONO

Binadamu yoyote anaeishi hapa duniani lazima awe na maono ya kitu gani anataka kwenye maisha yake, kitendo cha kukosa maono husababisha mtu kuishi ili mradi tu, mtu kama huyo huwa ana bidii yoyote na haonyeshi juhudi kwenye kile anachokifanya, mtu anapokosa maono maisha yake huishia kuwa ya kimaskini kwa sababu hataona haja ya kupambana ili afikie malengo Fulani, hivyo jitahidi uwe na maono ya nini unatarajia kuwa au nini malengo yako ya baadaye katika maisha yako.

 MADENI

Mlundikano wa madeni katika maisha ya mtu sio jambo zuri, madeni humfanya mtu kukosa raha katika maisha yake kamwe hautaweza kuwa huru kama una madeni na hasa kama yanazidi uwezo ulionao, lakini pia baadhi ya madeni ambayo watu hukopa huwa yanalipwa kwa riba  bado tena kunakuwa na kodi ambazo unapaswa uzilipe mwisho wa siku unajikuta unalipa pesa nyingi ukilinganisha na ulizozikopa 

Upukana na madeni, fanya kazi kwa bidii jenga tabia ya kutunza pesa zako mwenyewe ili zikusaidie kwenye shida ndogondogo za kimaisha ,

NENO LA MWISHO

Epuka kutumia hela zako kwa mkupuo kununua vitu vya gharama kama simu, luninga na vinginevyo kama kipato chako ni kidogo , wekeza taratibutaratibu, kisha ndio ununue na sio kuchukua mshahara wote na kuutumia mara moja, sababu kubwa ya ugumu wa maisha hutokana na udogo wa kipato hivyo ni muhimu kujifunza namna bora ya kutunza fedha, kuzitumia na namna gani utajikwamua kiuchumi ili kuweza kufika pale ambapo ulitamani ufike

 

 

Post a Comment

Previous Post Next Post